*MFAHAMU ELI COHEN....JASUSI NGULI KATIKA ULIMWENGU WA MAJASUSI*
Makala hii imeandaliwa na ***** kwa msaada wa Mitandao....
*Eli Cohen ni nani?*
Eliyahu Ben-Shaul Cohen (Eli Cohen) alizaliwa mjini Alexandria nchini Misri mwaka 1924 katika familia ya kiyahudi iliyokuwa ikiishi nchini humo. Katika ujana wake alishiriki katika mtandao wa siri ulikokuwa ukiwasafirisha wayahudi kutoka Misri kwenda Palestina iliyokuwa chini ya utawala wa kiingereza. Uhamiaji wa wayahudi ulikuwa ni maandalizi ya kuanzisha Taifa la Israel. Kazi hiyo aliendelea nayo hata baada ya kuzaliwa kwa Israel mwaka 1947. Ilipofika mwaka 1954 mamlaka za Misri zilifanikiwa kuharibu mtandao huo, huku Cohen na wenzake wakikamatwa na kuwekwa kizuizini. Hata hivyo hakukuwa na ushahidi wa kutosha kumfunga Cohen, na kwa hiyo aliachiwa huru.
Eli Cohen aliendelea kuishi nchini Misri hadi mwaka 1956, mara tu baada ya vita ya Suez kumalizika, akatimkia Israel. Huko alijiunga moja kwa moja na Intelijensia ya jeshi la Israel, Aman.
Kwa sababu ya ufasaha wake wa kuzungumza lugha za Kiarabu, Kiebrania na Kifaransa, alifanya kazi ya kutafsiri taarifa za siri hasa zilizohusu mataifa ya kiarabu.
Cohen hakuwa akibanwa sana na kazi za kiintelijensia kwa sababu alikuwa kama mtu wa kujitolea tu. Kutokana na historia yake ya kukamatwa nchini Misri alihisi kwamba hayupo makini na kazi hiyo. Ingawa ndani ya jumuiya ya kiintelijensia aliheshimiwa. Aliendelea kuishi maisha ya kawaida kama raia wengine, huku akipata na muda wa kutosha kwa familia, mke na watoto.
Haikuwa hivyo ilipofikia mei 1960 wakati mgogoro wa mpaka baina ya Israel na Syria ulipoanza. Israel ilihitaji Shushushu wa kuingia Damascus- Syria na kuvuna taarifa nyeti kutoka katika kitovu cha serikali ya Syria. Na jambo hilo lilikuwa la dharura.
Eli Cohen ndiye aliyekua mtu sahihi kwa kazi hiyo. Kikosi cha ushushushu namba 188 chini ya intelijensia ya jeshi kilipewa kazi hiyo. Kikosi hiki kilikuwa ni boresho la kikosi namba 131 cha awali.
Hatua ya kwanza ilikuwa kumtengeneza mtu tofauti ndani ya mwili wa Cohen, mtu ambaye ataishi mjini Damascus kama raia mzawa wa huko.
Kwahiyo, pamoja na udharura wa misheni hiyo, bado ilihitaji muda ili kuhakikisha kazi inafanyika kwa ufanisi wa kutosha.
Kumtengeneza mtu huyo, ilihitaji miezi sita na kwa kuanzia ilimpasa Cohen kuhudhuria mafunzo ya Quran nchini Israel ili awe mchangiaji mzuri katika mazungumzo yake na jamii ya waislamu atakaokutana nawo huko Syria.
Februari 1961, Cohen alisafiri hadi mjini Buenos Aires, Argentina kama mahala pa kuanzia (Base Country). Alitumia hati ya kusafiria ya nchi moja ya ulaya yenye jina tofauti alilotumia kwa muda nchini Argentina.
Enzi hizo Argentina ilikuwa chaguo la kuanzia kujenga historia ya uongo ya maisha ya mtu (cover story) anayetakiwa kufanya misheni katika nchi nyingine.
Miezi mitatu na nusu baadae, wakala kutoka kikosi cha 188 alitua nchini Argentina na kumkabidhi Cohen nyaraka zenye utambulisho mpya wa jina la Kamel Amin Taabeth, mfanyabiashara, raia wa Syria aliyezaliwa Lebanon.
Tangu hapo mtu anayeitwa Eliyahu Cohen, myahudi na mzaliwa wa Alexandria akapotea na kuibuka kama Kamel Amin Taabeth, mfanyabiashara mkubwa, raia wa Syria, mzaliwa wa Lebanon.
Tabeeth alikuwa na jukumu moja la kujichanganya na jamii ya watu wa Syria waliokuwa wakiishi nchini Argentina na kwengineko barani Amerika ya kusini. Misheni yake ilipaswa kuwa ya bajeti kubwa ili kumfanya kuwa mfanyabiashara tajiri, huku akikutana na Wasyria wenye ushawishi katika siasa za Syria na matajiri wakubwa wa Syria waliokuwa na biashara zao huko Amerika ya kusini.
Hadi kufikia mwanzo wa mwaka 1962, alikuwa amejiweka tayari kuingia katika nchi inayolengwa (Target Country) ya Syria.
Taabeth alisafiri kwa ndege kutoka Argentina mpaka Lebanon, kisha alitumia Taxi kuingia nchini Syria akiwa na mizigo mingi lakini mizigo muhimu ilikuwa miwili tu. Mmoja ni barua halisi ya kumtambulisha kwa mamlaka za Syria, iliyoandikwa na wafanyabiashara wa Syria wa huko Amerika ya kusini. Mzigo mwingine ni radio maalum ya mawasiliano kwa ajili ya kutuma taarifa nchini Israel.
Huko Damascus, Taabeth alikuwa mtu mpya lakini mpendwa na watu.
Kwa sababu ya utajiri wake aliweza kufanya tafrija nyingi huku akiwaalika maofisa wakubwa wa serikali ya Syria katika tafrija na shughuli zake mbalimbali. Wanasiasa na watu maarufu walifika nyumbani kwake na wakati mwingine aliwaandalia wasichana warembo kwa ajili ya kuwaburudisha wageni wake.
Kwa bahati tu, baada ya kitambo kidogo, mmoja kati ya marafiki zake wa mjini Buenos Aires, Major Amin Al-Hafez, alikuja kuwa Rais wa Syria.
Tabeeth alijijengea umaarufu mkubwa na ukaribu na maafisa wa vyombo vya dola. Alialikwa mara kwa mara katika maofisi ya dola na kambi za kijeshi. Hatimaye akawa mtu wa karibu na Rais Amin Al Hafez.
Kila alipotembelea vituo vya kijeshi, Tabeeth alichota taarifa na kuzituma nchini Israel kwa mawasiliano ya siri ya kutumia radio maalum. Alipata ramani ya vituo vya jeshi la Syria vilivyo katika miinuko ya Golan, mpakani mwa Israel (wakati huo), alituma taarifa kuhusu aina na idadi ya silaha kubwa, majina ya marubani wa ndege za kivita na maofisa wakubwa wa jeshi, historia zao, maisha yao na tabia zao, mipango na mbinu za kivita za Syria, pamoja na maeneo ya udhaifu wa Israel ambayo Syria ilikuwa ikiyajua.
Maurice Cohen, mdogo wake Eli Cohen/Taabeth ndiye aliyekuwa akipokea na kutafsiri taarifa hizo kutoka kwa mdogo wake aliyekuwa akifanya kazi ya kujiandaa kufa huko Damascus.
Kabla ya hapo, ndugu hawa hawakufahamu kuwa wote ni watumishi wa intelijensia ya Israel. Eliyahu alimwambia mdogo wake anasafiri kwenda nje ya nchi kununua kompyuta kwa ajili ya wizara ya ulinzi. Hata wakati wa mawasiliano ya kutoa taarifa kutoka Syria kwenda Israel hawakuwa wakifahamu kuwa ni ndugu kwakuwa walitumia majina maalum ya siri (Code names)
Kifo cha Cohen.
Novemba 1964 Cohen alirudi kwa siri nchini Israel kusabahi familia yake. Kisha aliamua kukutana na viongozi wa intelijensia wa Israel na kuwaeleza kuwa anahisi hatari. Kiongozi wa intelijensia ya kijeshi wa Syria, Kanali Ahmed Suedani alikuwa anamuhisi Cohen.
Cohen alitanabaisha kuwa anataka kurudi nyumbani baada ya kazi ya karibu miaka minne ya kwenye "baridi kali". Alihisi kifo kinamkaribia. Akiwa Israel ndipo yeye na mdogo wake Maurice walipogundua kuwa walikuwa wakibadilishana taarifa kutoka Syria kwenda Israel. Lakini hakukuwa na tija ya kujadili zaidi jambo hilo.
Kwa bahati mbaya, aliyekuwa na jukumu la kuratibu shughuli za Cohen (Case handler) huko Israel hakutilia maanani kauli za Cohen. Wakati huo, mgogoro wa mpaka ulikuwa umeibuka upya, na vita ilikuwa inakaribia. Jeshi la Israel lilihitaji mtu wa kuchota taarifa kutoka Damascus wakati huo kuliko wakati wowote. Hakukuwa na mtu mwingine zaidi ya Cohen, na kwa hiyo Cohen alitakiwa kurudi katika kituo chake cha kazi mara moja.
Pengine ni kwa sababu ya kuchoshwa na kazi hiyo ya siri, au kwa sababu zingine Cohen alisahau kanuni ya busara. (Rule of prudence) na hivyo akawa anatuma taarifa bila ratiba maalum. Kwa muda wa wiki 5 alifanya mawasiliano mara 31. Na kwa sababu ya unyeti wa taarifa hizo, Wapokezi wa taarifa huko Israel, akiwemo Maurice aliyekuwa anatafsiri taarifa hizo, walijisahaulisha na kushindwa kumuonya.
Majasusi wa Sovieti (Urusi ya leo) walinasa mawasiliano hayo na wakati huo Syria ilikuwa rafiki wa Soviet. Baadae majasusi hao wa Soviet walimpa taarifa kiongozi wa intelijensia ya jeshi la Syria, Kanali Ahmed Suedani na kumsaidia kunyaka mawasiliano ya Cohen/Taabeth aliyokuwa akifanya na Israel. Januari 18, 1965 vijana wa Kanali Suedani walivamia ndani ya nyumba ya Cohen/Taabeth na kumkuta akifanya mawasiliano na Israel. Akadakwa.
Kulikuwa na hali ya mshtuko mjini Tel Aviv, Isael. 'Mtu' wa nchi ingine aliyekuwa Syria alitoa taarifa ya kukamatwa kwa Eli Cohen siku moja baadae.
Serikali ya Israel ilianza mara moja mipango ya kumkomboa Cohen kutoka Syria, au hata ikibidi kumuepusha na kifo.
Mwanasheria mahiri wa Kifaransa alikodishwa na kuomba msaada wa kidiplomasia kutoka jumuia ya ulaya na kutoka kwa Papa Paulo IV huko Vatican. Pia serikali za Canada, Ubelgiji na Ufaransa, kwa kuombwa na Israel ziliishawishi Syria kuachana na adhabu ya kifo kwa Cohen.
Hata hivyo, mnamo tarehe 18 Mei 1965, Cohen alinyongwa hadharani katika eneo la mraba wa Marjeh, mjini Damascus.
Kabla ya kunyongwa Cohen alimuandikia mkewe Nadia ujumbe mfupi akisema "Nakuomba usiomboleze ee Nadia kwa mambo yaliyopita. Jitazame mwenyewe na kuitafuta kesho mpya". Pia kabla ya kunyongwa, Cohen aliomba kukutana na kiongozi wa kidini wa huko Syria, "Rabbi" Nissim Andabo ambaye aliruhusiwa kuongozana naye alipokuwa akipelekwa kunyongwa.
Tangu wakati huo, Nadia amekuwa akiomba mwili wa mumewe urudishwe nchini Syria kwa ajili ya maziko, kaka yake Eli Cohen, Maurice kabla ya kufariki kwake mwaka 2006, aliwahi kufanya kampeni kadhaa za kutaka kurudishwa mwili wa kaka yake, akisaidiwa na serikali ya Israel bila mafanikio.
Septemba 20, 2016 video ya kunyongwa kwa Cohen ilirushwa katika mtandao wa facebook, haikuwa ikijulikana kama video hiyo ipo. Mamlaka za Israel zilithibisha kuwa Video hiyo si ya kutengenezwa bali ni halisi.
Julai 5, 2018, Shirika la ujasusi la Israel, Mossad wametangaza kuipata saa ya mkononi ya Eli Cohen iliyotangazwa kuuzwa huko Syria. Nadia, mke wa Cohen mwenye miaka 82 bado anaomboleza hadi leo, anaamini siku moja mifupa ya mume wake itarudishwa kuzikwa Israel.
Katika sherehe za kuonesha Saa hiyo, alikuwapo kiongozi wa Mossad wa sasa, Yosi Cohen.
Saa hiyo itahifadhiwa katika makao makuu ya Shirika la Mossad, Tel Aviv, Israel.
Picha zipo ukurasa wa twitter wa @jashyie
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni